ads here

Tanzania yaongoza maharage EAC.👉 HabarileoJul 5, 2020

advertise here




UZALISHAJI wa maharage nchini unapaswa kuongezeka ili kukidhi soko la ndani na nje ya nchi, kwa kuwa hivi sasa mahitaji ya nchi ni tani milioni moja lakini yanazalishwa tani milioni 1.2.

Mratibu wa zao la maharage nchini kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo (Tari) Kituo cha Ilonga kilichopo Mbeya, Dk Rose Mongi alisema hayo alipozungumza na HabariLeo kuhusu majaribio ya maharage yanayoendelea kituoni hapo.

Dk Mongi alisema Tanzania inaongoza kwa kilimo cha maharage katika Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) hivyo mahitaji ni makubwa kwani hivi sasa yanayozalishwa nchini yanauzwa katika nchi za Zambia, Kenya, Congo, Malawi, Rwanda na Burundi.

Alisema kwa kuwa mahitaji ni makubwa, Tanzania bado ina fursa ya kuongeza uzalishaji huo, hivyo kituo cha Uyole kinafanya utafiti katika zao hilo ili kuhakikisha watanzania wanapata mbegu bora itakayowawezesha kujikimu na kupata ziada.

“Tunafanya utafiti wa aina nyingi mpaka sasa tumeshatoa mbegu 42 tofauti tofauti, tunasema maharage kwa ajili ya mahitaji ya ndani hayajatosheleza kwa sababu yanauzwa nje ya nchi,” alisema Dk Mongi.

Alisisitiza katika kituo hicho, majaribio yanaendelea ili kupata mbegu bora zaidi zikiwemo zinazostahimili ukame pamoja na joto kali, hivyo mwaka huu wanatarajia kutoa mbegu aina tatu.

Alitaja baadhi ya mbegu bora za maharage zinazopendwa kuwa ni Njano Uyole, Calima Uyole, Uyole 18, Uyole 03, Uyole 99, Uyole 04 na Nyeupe Uyole.

Alisema changamoto zilizopo kwa zao hilo ni magonjwa ya majani, madoa pembe, ndui ya maharage, kutu na ugonjwa wa mizizi, wadudu ni inzi wa maharage na wadudu waharibifu kwenye maghala kama bungua wa maharage.

Mkurugenzi Mkuu wa TARI, Dk Geofrey Mkamilo alisema taasisi hiyo inahakikisha teknolojia mbalimbali ambazo zimegunduliwa zinawafikia wakulima kwa kuwa itakuwa haina maana zisipokuwa na mchango wowote kwa wakulima na wadau wengine katika mnyororo wa thamani. “Kilimo kichangie uchumi wa kaya na taifa kwa ujumla ili mkulima aachane na kilimo cha kujikimu na kulima cha kibiashara,” alisema.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa TARI, Dk Yohana Budeba alisema kilimo ni uti wa mgongo hapa nchini hivyo anaipongeza serikali kwa kuanzisha TARI kwa kuwa imeleta mageuzi ya kilimo nchini kwa kujibu changamoto za wakulima kupitia utafiti unaofanywa.

Aliwataka wananchi kuanza kutumia teknolojia ambazo watafiti wamezitambua ili kupata tija kwenye mazao yao.

Mkurugenzi wa Kituo cha Uyole, Dk Tulole Bucheyeki alisema wanazalisha mbegu bora za zao hilo na kutoa utaalamu, hivyo umefika wakati wa wakulima kulima kibiashara. Pia alisema TARI imeamua kufanya utafiti kwa juhudi kubwa ili kuwatoa wakulima katika kilimo cha kizamani na kuwafundisha cha kisasa kinachotumia teknolojia bora.
Advertisement
BERIKAN KOMENTAR ()